Thursday 20 October 2016

MAPATO YA MINADA WILAYANI SERENGETI YAONGEZEKA.

Habari toka Kitengo cha Habari na Mawasiliano.
HALMSHAURI YA WILAYA YA SERENGETI.


Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti, Mhe. Juma Porini Keya akitoa risiti kwa kutumia kifaa cha POS.

“Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti imefanikiwa kuongeza mapato yatokanayo na minada mbali mbali inayofanyika ndani ya Wilaya”

Hayo yamesemwa na Terry Hurson ambae ni Kaimu Mtunza Fedha wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti alipokuwa anazungumza na Waheshimiwa Madiwani wanaounda Kamati ya Fedha, Uongozi na Mipango waliofanya ziara katika Mnada wa Kijiji cha Rung’abure kilichopo Kata ya Rung’abure.

Ziara hiyo ya ukaguzi ni mwendelezo wa taratibu zilizowekwa na Serikali kwa kuwahusisha Waheshimiwa Madiwani wanaounda Kamati ya Fedha, Uongozi na Mipango kutembelea miradi kila baada ya miezi mitatu (Robo Mwaka wa Serikali)

Kamati ya Fedha Uongozi na Mipango inayoongozwa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti, Juma Porini Keya pamoja na Katibu wa Kamati hiyo ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti Juma Hamsini pamoja na wajumbe wa Kamati walijionea jinsi ukusanyaji wa mapato unavyofanyika kwa kutumia vifaa vya kieletroniki (POS) vinavyotumika pia kutoa risiti za malipo. “Mapato ya Minada yameongezeka kutokana na kuzuia mianya ya ukwepaji wa kodi na matumiz ya POS” alisema Terry Hurson. Aliongeza kwa kusema "kipindi cha mzabuni mapato yatokanayo na mnada wa kijiji cha Rung'abure yalikua ni Tshs Milioni 2.4 kwa mwezi na sasa tunakusanya wastani wa Tshs Milioni 3.2"

Ukusanyaji wa mapato unafanywa na watumishi wa Serikali, hii ni baada ya Serikali ya awamu ya tano ikiongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli kuzitaka Halmashauri zote nchini kukusanya mapato na kuacha kutumia wazabuni katika kukusanya mapato kwenye masoko na minada.

                                                             MATUKIO KATIKA PICHA
Kutoka Kushoto Mhe. Juma Porini Keya, katikati ni Bw. Terry Hurson (Kaimu Mtunza Fedha) kushoto ni Charles Ghati (Mkusanyaji wa Mapato) katika mnada wa Rung'abure.


Wafanyabiashara katika mnada wa kijiji cha Rung'abure wakifanya malipo.
Huduma za chakula pia hupatikana.


No comments:

Post a Comment